Header Ads

Chelsea wananichukulia kama mhalifu - Costa



https://ichef-1.bbci.co.uk/news/660/cpsprodpb/8459/production/_97318833_gettyimages-618393984.jpg

SAO PAULO- MSHAMBULIAJI matata, Diego Costa amesema Chelsea wamekuwa wakimchukulia kama ‘mhalifu’ na akathibitisha kwamba bado anataka kurejea Atletico Madrid.
Costa (28) aliichezea Chelsea mara ya mwisho kwenye fainali ya Kombe la FA mnamo Mei mwaka huu, alitumiwa ujumbe na kocha wa timu hiyo, Antonio Conte mwezi Juni kufahamishwa kwamba hakuwa kwenye mipango ya msimu ulioanza siku juzi.
Costa alisema sasa klabu hiyo inamshurutisha kurejea akafanye mazoezi na wachezaji wa akiba.
“Ni kwa nini hawataki kuniacha niondoke iwapo hawanitaki? Lazima nifanye yale inanibidi kuyafanya. Lazima nifikirie kuhusu maslahi yangu. Nimekuwa mvulana mzuri hapa na nilijaribu kufanya kila kitu sawa. Mapenzi yangu ni kwenda Atletico,” alisema Costa ambaye anaamini Conte ndiye anayemchongea.
“Januari, mambo yalifanyika kati yangu na kocha. Nilikuwa nimekaribia kutia saini mkataba mpya, lakini akasimamisha hilo. Nashuku meneja alihusika. Aliomba hilo lifanyike.
“Mawazo yake ni wazi na hayabadiliki. Nimeona yeye ni mtu wa aina gani. Ana mtazamo wake na huo hautabadilika.
“Namheshimu kama kocha. Amefanya kazi nzuri na naona hilo, lakini kama binadamu, la. Si mkufunzi ambaye ana uhusiano wa karibu na wachezaji. Hukaa mbali. Hana sifa za kuhusiana vyema na wachezaji,” alisema Costa.
Juni mwaka huu, Costa alitumiwa ujumbe mfupi wa maneno (sms) na Conte kufahamishwa hangekuwa kwenye mipango ya timu hiyo.
“Sijaufuta ujumbe huo wa simu. Watu wakinituhumu kwamba nasema uongo, naweza kuwaonesha. Ujumbe huo ulikuwa wazi, alisema simo kwenye mipango yake na akanitakia kila la kheri siku zijazo. Weka kikomo hapo,” alieleza Costa.
Mshambuliaji huyo wa Hispania alipewa muda zaidi kupumzika na Chelsea mwezi uliopita, lakini sasa anasema anaadhibiwa kwa hilo.
Anasema anatozwa faini kwa kutokuwa kwenye klabu muda huo, na amesema anafikiria kwenda kortini au kujaribu kumaliza sehemu iliyosalia ya mkataba wake bila ujira nchini.
“Unajua meneja hanitaki. Nasubiri Chelsea waniachilie huru. Sitaki kuondoka. Nilikuwa na furaha. meneja asipokutana, ni lazima uondoke,” Costa alisema.
Costa ambaye ni mzaliwa wa Brazil lakini huchezea timu ya taifa ya Hispania, alijiunga na Chelsea kutoka Atletico Madrid kwa pauni milioni 32 (sh bilioni 92.8) mwaka 2014.
Alikaa misimu minne Atletico na alikuwa amedokeza kwamba huenda akarejea katika klabu hiyo.
BBC

No comments

Powered by Blogger.