Header Ads

Bolt: Nilikaribia kulia wakati nikiwaaga wanariadha na mashabiki



https://nbcolympictalk.files.wordpress.com/2017/08/831123368-e1502662063924.jpg?w=610&h=343&crop=1

LONDON- MWANARIADHA mahiri wa Jamaica, Usain Bolt amesema hakuna wakati mgumu aliowahi kukabiliana nao maishani mwake kama alipokuwa akiaga mashabiki wake.
Anasema wakati ‘anasema kwaheri kwa kila kitu’ na alikaribia kumwaga chozi, baada ya kufika kikomo cha maisha ya uanariadha katika mashindano ya ubingwa wa dunia jijini hapa.
Bolt, 30, mshindi wa medali ya dhahabu mara nane katika Olimpiki, amestaafu rasmi riadha baada ya kung'aa na kujizolea umaarufu mkubwa.
“Inasikitisha kwamba inanilazimu kuondoka sasa. Nilikuwa nasema kwaheri kwa mashabiki na kwaheri kwa mashindano niliyokuwa nashiriki pia,” alisema raia huyo wa Jamaica, ambaye alikimbia kuzunguka uwanja kuaga jana usiku wa kufungwa kwa mashindano hayo.
Alipoulizwa iwapo atarejea kushindana tena, alijibu: “Nimewaona watu wengi wakistaafu na kurudi tena, halafu hali yao inakuwa mbaya zaidi au wanajiaibisha. Sitakuwa mmoja wa watu hao.”
Bolt alishinda shaba mbio zake za mwisho za mita 100, kisha akaumia na kushindwa kumaliza mbio za kupokezana vijiti za meta 4x100 Jumamosi usiku.
Hii ina maana kwamba bingwa huyo wa dunia mara 19, ambaye Lord Coe alimfananisha na Muhammad Ali, aliondoka kwa njia isiyo ya kawaida wakati akisaidiwa kuondoka uwanjani na wenzake, akiwa hawezi kusimama vyema wima baada ya kuumia.
“Kwangu, sidhani mashindano haya yatabadilisha yote niliyoyafanya. Nakumbuka baada ya kushindwa mbio za meta 100, kuna mtu alinijia na kuniambia, 'Usain, usiwe na wasiwasi, Muhammad Ali alishindwa pigano lake la mwisho, hivyo usisikitike sana kuhusu hilo.
“Nimedhihirisha ustadi wangu, mwaka baada ya mwaka. Katika kipindi changu chote nilichoshiriki mbio hizi. Nilikuwa nasema kwaheri kwa kila kitu na nilikaribia kulia. Nilikaribia sana, lakini machozi hayakutoka,” alisema Bolt.
BBC

No comments

Powered by Blogger.