Header Ads

Bunge la Iran lapitisha muswada kuboresha makombora



https://ichef.bbci.co.uk/news/660/cpsprodpb/1333B/production/_97315687_iranmissiles.jpg

TEHRAN- Bunge la Iran, limepitisha muswada wa kutenga zaidi ya dola za Marekani milioni 500 (sh trilioni 1.1), kwa ajili ya mradi wake wa kuboresha makombora.
Iran inajibu vikwazo vya karibuni kabisa, vilivyowekwa na Marekani dhidi yake kutokana na programu hiyo.
Vyombo vya habari nchini, vinasema fedha hizo zinakusudiwa kupambana na vile vilivyoitwa vitendo vya kigaidi vya Marekani katika Mashariki ya Kati.
Muswada huo utaweka vikwazo dhidi ya wanajeshi pamoja na maofisa wa ujasusi wa Marekani.
Mpatanishi mkuu wa Iran katika mazungumzo kuhusu mradi wake wa nyuklia, Abbas Araqchi, amesema muswada huo mpya umeungwa mkono na Wizara ya Mambo ya Nje, na kwamba hauendi kinyume na makubaliano ya mwaka 2015, yaliyozuia mradi wa nyuklia wa Iran.
Makubaliano kuhusu programu ya nyuklia kati ya Iran na mataifa sita yenye nguvu duniani ikiwemo China, Urusi na Uingereza, yanaonekana kwa kiwango kikubwa kama njia mwafaka ya kuizuia Iran kuunda zana za nyuklia.
Makubaliano hayo yalisababisha vikwazo vibaya kwa uchumi wa Iran kuondolewa, ili nchi hiyo ipate kupunguza programu zake za nyuklia.
BBC

No comments

Powered by Blogger.