Header Ads

Mwanamke aliyevaa nguo fupi kuchunguzwa Saudia



Mwanamke aliyevalia sketi fupi Saudia achunguzwa

RIYADH- MAMLAKA nchini, zinamchunguza mwanamke mmoja aliyechapisha kanda yake ya video akiwa amevalia sketi fupi na tishet iliyo wazi hadharani.
Mwanamke huyo ambaye ni mwanamitindo aitwaye Khulood, alisambaza video hiyo akitembea katika ngome ya kihistoria ya Ushayqir.
Kanda hiyo ilizua hisia na mjadala mkali, huku wengine wakitaka akamatwe kwa kuvunja sheria kali ya uvaaji wa mavazi nchini. Raia wengine walimtetea mwanamke huyo wakimsifu kwa ujasiri wake.
Wanawake nchini ni sharti wavae nguo zisizowabana na ndefu, zajulikanazo kama ‘abaya’ hadharani pamoja na kitambaa kichwani. Pia, hawaruhusiwi kuendesha magari na hutengwa na wanaume wasio kuwa na uhusiano wa kifamilia.
Katika video hiyo iliosambazwa katika mtandao wa Snapchat wikendi iliyopita, Khulood anaonekana akitembea katika barabara isiyo na watu katika ngome hiyo ya historia ya Ushayqir yapata kilometa 155, Kaskazini mwa mji huu wa Riyadh mkoani Najd.
Najd ni miongoni mwa maeneo ya kihafidhina nchini. Ni eneo ambalo mwanzilishi wa Wahabi alizaliwa katika karne ya 18.
Video hiyo ilichukuliwa na watumiaji wa mtandao wa Twitter nchini, ambapo kulikuwa na mjadala mkali kati ya wale wanaoamini Khulood angepaswa kuadhibiwa na wengine waliosisitiza kuwa anafaa kuachwa kuvaa anachotaka.
BBC

No comments

Powered by Blogger.