Header Ads

Trump aanza kuandaa fedha za kampeni ya urais 2020



Image result for Trump in 2020 fundraising
WASHINGTON DC- RAIS Donald Trump ameandaa hafla ya kuchangisha fedha ambazo zinadaiwa kuwa zitatumika kwenye kampeni za urais za mwaka 2020 katika hafla ambayo imeandaliwa katika hoteli moja mjini hapa.

Hata hivyo, hafla hiyo ilitiwa doa na waandamanaji ambao walimkaripia kiongozi huyo wakisema kwa sauti ‘Aibu!’ alipowasili kuhudhuria hafla hiyo. Kwenye hafla hiyo, kila aliyehudhuria alikuwa analipa $35,000 (sh milioni 77).
Wengi wa waandamanaji walikuwa hawajaridhishwa na mpango wa bima ya afya wa chama cha Republican, na walikuwa na mabango yenye ujumbe ‘Bima ya afya, na wala si kupunguzwa kwa kodi.’
Hoja ya kwamba hafla hiyo ilifanyika katika hoteli ya Trump International, imeibua tena wasiwasi kuhusu muingiliano wa maslahi kati ya majukumu ya Trump kama rais na biashara zake.
Richard Painter, ambaye alihudumu katika ikulu ya White House kama mwanasheria aliyehusika na masuala ya maadili wakati wa utawala wa Rais George W Bush, amesema haikubaliki kwa rais kuonekana akifaidika kifedha kutoka kwa hafla ya aina hiyo.
Amesema rais huyo angechagua hoteli nyingine na wala si moja ya hoteli zake.
Lakini, Kathleen Clark, Profesa wa masuala ya uanasheria anayeangazia fani ya maadili katika Chuo Kikuu cha Washington mjini St. Louis, aliambia USA Today, kwamba Trump hakuvunja sheria zozote.
Haijabainika bado, iwapo hoteli hiyo ililipwa kuwa mwenyeji wa hafla hiyo. Maofisa wa kamati ya taifa ya chama cha Republican walitarajia kuchangisha takriban dola milioni 10 (sh bilioni 22), na kulikuwa na nafasi 300 zilizokuwa zinauzwa.
Hata hivyo, fedha zote hazitatumiwa kwa kampeni ya Trump 2020 - kuna nyingine zitatumiwa na chama cha Republican. Ni jambo lisilo la kawaida kwa rais kuanza kuchangisha fedha za kutetea kuchaguliwa tena mapema hivyo muhula wake wa kwanza.
Trump amehudumu kama rais kwa miezi mitano pekee.
“Bila shaka atapigania kuchaguliwa tena,” msemaji wa White House, Sarah Huckabee Sanders aliwaambia wanahabari jana.

No comments

Powered by Blogger.