Header Ads

Bobi Wine ashinda ubunge Uganda



Mwanamuziki Bobi Wine akamatwa Uganda
KAMPALA- MWANAMUZIKI mashuhuri wa mtindo wa Afrobeats nchini, Robert Kyagulanyi Ssentamu, maarufu Bobi Wine, ameshinda ubunge katika uchaguzi mdogo nchini.

Wine (pichani), ambaye aliwania nafasi hiyo kama mgombea huru, aliwashinda wagombea wengine wanne katika jimbo la Kyadondo Mashariki katikati mwa Uganda.
Taarifa iliyotolewa na gazeti la Serikali la New Vision, ilieleza kuwa Wine alipata kura 25,659 kati ya kura 33,310 zilizopigwa. Gazeti hilo lilisema baada ya kutangazwa mshindi, aliahidi kuangazia zaidi kuwaunganisha raia.
“Jambo langu la kwanza ninalotaka kulifanya, ni kufanikisha maridhiano kati ya viongozi wa Kyadondo Mashariki. Ninataka siasa zitulete pamoja kama ambavyo muziki ufanyavyo,” alisema Wine.
Mwanamuziki huyo alikamatwa na polisi na kuhojiwa kwa muda, kabla ya kuachiliwa siku chache zilizopita. Kiti hicho cha ubunge kiliachwa wazi, baada ya mahakama kuamua kuwa uchaguzi uliofanyika mapema mwaka jana haukufuata kanuni na sheria za uchaguzi.
Kiongozi wa chama cha upinzani cha FDC, Kizza Besigye amempongeza mwanamuziki huyo kwenye Twitter.
Bessigye aliandika kwamba: “Ushindi mkubwa kwa Mheshimiwa Bobi Wine. Hongera - Nguvu za Raia!! Ndio maana watu wa Wakiso hawakuruhusiwa kupiga kura mwaka 2016.”
Wine alianza muziki mapema miaka ya 2000. Baada ya uchaguzi mkuu wa 2016, alitoa wimbo kwa uitwao Situka, ambao maana yake ni inuka au zinduka kwa Kiluganda.
Kwenye wimbo huo, anatoa mwito kwa raia wa Uganda kushiriki kwenye vita dhidi ya rushwa na ukiukaji wa haki nchini mwao.
BBC


No comments

Powered by Blogger.