Ujerumani yakataa kumwachia jasusi wa Uswisi

KARLSRUHE- MAHAKAMAya Juu mjini hapa, imetupilia mbali ombi
la kumwachia raia mmoja wa Uswisi ambaye anashikiliwa kwa madai ya kufanya
upelelezi nchini.
Mwanaume huyo ambaye ametambuliwa kama Daniel M
(54), alikamatwa mnamo April mwaka huu hotelini mjini Frankfurt kwa madai ya
kufanya upelelezi nchini tangu mwaka 2012.
Taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ilieleza kuwa ombi la kumwachia jasusi huyo
limekataliwa na ataendelea kushikiliwa.
Upande wa mawakili wa Serikali, uliieleza mahakama
hiyo kuwa Daniel M. amekuwa akipokea maagizo ya msingi kutoka kwa Shirika la
Ujasusi la Uswisi (FIS) lakini hayo yaliyosababisha akamatwe yalikuwa muhimu
zaidi na yalikuwa kinyume na matakwa ya Serikali ya Ujerumani.
Inadaiwa kuwa jasusi huyo alipewa jukumu la
kuwabaini wapelelezi watatu wa Idara ya Kodi ya Ujerumani, ambao walinunua CD
zenye taarifa za watu wenye akaunti za benki za kigeni kwenye mataifa yenye
misamaha ya kodi kama Uswisi.
Taarifa alizokusanya Daniel M. zinadaiwa kuisaidia
Uswisi kufungua kesi dhidi ya wapelelezi hao, kwa kuvunja sheria za kibenki za
Uswisi na kufanya ujasusi wa kiuchumi.
Mbali na hayo, mawakili hao wa Serikali waliieleza
mahakama kwamba jasusi huyo wa Uswisi anadaiwa kupandikiza kifaa maalum cha
kukusanya taarifa kwenye jengo la Wizara ya Fedha ya Ujerumani, madai ambayo
mtuhumiwa aliyakanusha.
Hata hivyo, inaelezwa kwamba mara baada ya
kukamatwa kwa jasusi huyo, Ujerumani na Uswisi zilisaini haraka makubaliano ya
kusitisha ujasusi baina yao.
The Local
No comments