Header Ads

Wazazi wataka mtoto wao aitwe Allah

ACLU lawsuit


GEORGIA, Marekani
WANANDOA wawili jimboni hapa, wamewasilisha kesi mahakamani baada yao kuzuiwa kumpa mtoto wao jina Allah.
Wizara ya Afya ya Umma ya jimbo ilikataa kumpa msichana huyo wa umri wa miezi 22 cheti cha kuzaliwa kwa sababu ya jina lake. Elizabeth Handy na Bilal Walk wanasema haikubaliki kwamba sasa mtoto wao ameachwa kirasmi akiwa hana jina.

Lakini maofisa wa Serikali wanasema jina la ukoo la mtoto huyo ZalyKha Graceful Lorraina Allah linafaa kuwa Handy, Walk au majina yote mawili.
Allah ni jina la Mungu kwa Kiarabu.
Shirika la Haki za Raia Marekani (ACLU) tawi la Georgia limewasilisha kesi kwa niaba ya familia hiyo katika Mahakama Kuu ya wilaya ya Fulton. Baba yake msichana huyo, aliambia gazeti la Atlanta Journal-Constitution kwamba aliamua kumpa jina Allah kwa sababu ni jina ‘adilifu’.
"Huu ni ukiukaji wazi wa haki zetu," Walk alisema kuhusu hatua ya jimbo kukataa kutambua jina hilo.
Hata hivyo, mawakili wa Wizara ya Afya ya Umma ya jimbo wanasema sheria za Georgia ‘hutaka jina la ukoo la mtoto liwe la baba au mama yake mtoto kwa ajili ya hati ya kwanza rasmi ya kuzaliwa (kwa mtoto).’
Kwenye barua kwa familia hiyo, maofisa wa Serikali walisema jina la ukoo la ZalyKha linaweza kubadilishwa baadaye kupitia ombi kwa Mahakama Kuu ya jimbo.
Hata hivyo, hilo linaweza kufanyika tu baada ya cheti cha kwanza cha kuzaliwa kwa mtoto huyo kutolewa.
Kwa mujibu wa kesi iliyowasilishwa kwa niaba ya familia hiyo, wanandoa hao ambao hawajafunga ndoa rasmi wana mtoto wa kiume aliyepewa jina Masterful Mosirah Aly Allah.
ACLU wanasema bila kupata cheti cha kuzaliwa, itakuwa vigumu kwa wazazi hao kupata nambari rasmi ya utambulisho kwa ajili ya kupokea huduma kutoka kwa Serikali. Wanahofia kwamba huenda utambulisho wa msichana huyo, pamoja na haki zake kama raia wa Marekani zikatiliwa shaka.
ACLU wamesema hatua ya jimbo hilo kukataa kutimiza maombi ya familia hiyo ni mfano wa serikali kuvuka mipaka na kutofuata katiba.
“Wazazi ndio huamua jina la mtoto wala siyo jimbo. Ni jambo rahisi sana” alisema wakili wa familia hiyo, Michael Baumrind.
 

No comments

Powered by Blogger.