Header Ads

Watu 600 hawajulikani walipo Sierra Leone



https://ichef-1.bbci.co.uk/news/660/cpsprodpb/4CF4/production/_97400791_1c115c73-6753-4308-8047-df235159d1be.jpg

FREETOWN- TAKRIBAN watu 600 wametoweka mjini hapa, kufuatia maporomoko ya matope na mafuriko yaliyotokea katika maeneo kadhaa mjini hapa.  
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Rais Ernest Bai Koroma, Abdulai Baraytay, ilieleza maporomoko hayo yaliyotokea katika baadhi ya sehemu mjini hapa yamesababisha kutoweka kwa watu hao ambapo jana ilipatikana miili 270.
Awali, Rais Koroma aliomba usaidizi wa dharura akisema jamii nzima ilikuwa imeangamia.
Takriban watu 400 wamethibitishwa kufariki dunia, kutokana na maporomoko hayo ya eneo la Regent na mafuriko yaliyotokea katika maeneo mengine mjini hapa.
Shjrika la Msalaba Mwekundu limeonya kuwa, hakuna muda wa kutosha kuweza kuwaokoa manusura. Maziko ya pamoja ya waathiriwa yanatarajiwa kufanyika leo ili kupunguza idadi ya miili katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Baraytay aliiambia BBC kwamba, miili ilikuwa ikitolewa katika matope hayo na vifusi na kuongeza kuwa jamii nzima inaomboleza.
“Wapendwa wengine wametoweka, takriban zaidi ya watu 600,” alisema Baraytay.
Umoja wa Mataifa (UN) umesema kwamba, wafanyakazi wake nchini wamekuwa wakisaidia katika juhudi za kuwaokoa manusura.
“Mikakati inawekwa kuzuia mlipuko wowote wa magonjwa yanayosababishwa na maji kama vile kipindupindu, homa ya manjano na kuharisha,” alisema Msemaji wa UN, Stephane Dujarric.
Nyumba za jamii zilizokuwa zikiishi juu ya mlima ziliangamia, baada ya upande mmoja wa mlima wa Sugar Loaf kuporomoka kufuatia mvua kubwa mapema siku ya Jumatatu.
Waathiriwa wengi walikuwa wakilala wakati wa mkasa huo.
Rais Koroma alizuia machozi alipotembelea eneo la Regent siku ya Jumatatu na kusema kuwa uharibifu huo umepita kiasi.
''Jamii nzima imeangamia tunahitaji msaada wa dharura'', alisema.
BBC

No comments

Powered by Blogger.