Header Ads

Waandamana kushinikiza uchunguzi kifo cha ofisa IEBC



Waandamanaji

NAIROBI- WATETEZI wa haki za kibinadamu wameandamana katika uwanja wa Uhuru Park, kushutumu kuuawa kwa ofisa wa ngazi za juu wa Tume ya Uchaguzi Kenya (IEBC), Christopher Msando.
Msando alitoweka Ijumaa na mwili wake ukapatikana ukiwa umetupwa viungani mwa jiji hili Jumamosi asubuhi. Mwili wake ulitambuliwa jana katika chumba cha kuhifadhia maiti cha City.
George Kegoro kutoka shirika lisilo la kiserikali la Tume ya Haki za Kibinadamu Kenya (KHRC), amesema wana wasiwasi kwamba mauaji ya Msando yatazua mtafaruku uchaguzi mkuu unapokaribia.
Waandamanaji walibeba mabango wakihimiza umuhimu wa tume ya uchaguzi IEBC, kutoingiliwa.
Wamesema sababu pekee ya kumuua ofisa huyo aliyekuwa akisimamia mfumo wa teknolojia wa uchaguzi katika tume hiyo, ni kuingilia uchaguzi wenyewe na kwamba hilo huenda likachochea ghasia.
Waandamanaji hao walipanga kuandamana hadi ofisi za Mkuu wa Polisi, Joseph Boinnet na makao makuu ya IEBC.
Mwenyekiti wa IEBC, Wafula Chebukati, kupitia taarifa baada ya kutambuliwa kwa mwili wa Msando, alitoa mwito kwa polisi kufanya uchunguzi wa kina kubaini chanzo cha kifo chake.
“Tume itamteua wakili huru wa kushirikiana na Mkuu wa Polisi katika uchunguzi. Tunataka haki kwa Chris, Haki kwa IEBC na Haki kwa Taifa,” alisema Chebukati.
Chebukati alimuomba mkuu wa polisi kuimarisha ulinzi kwa makamishna na maofisa wakuu wa tume hiyo.
BBC.

No comments

Powered by Blogger.