Header Ads

Mkulima kumzawadia ng’ombe wake wa pekee Rais Kenyatta



THARAKA- MKAZI mmoja wa kijiji cha Nkondi, amepanga kusafiri umbali wa kilometa 500 hadi kufika Ikulu ya Kenya jijini Nairobi, kwa ajili ya kumpa zawadi Rais Uhuru Kenyatta.
Mwanaume huyo, Duncan Mutiria mwenye umri wa miaka 40, amesema anapanga kutembea umbali huo mrefu ili kumpa Rais Kenyatta zawadi ya ng’ombe dume wa pekee aliyenaye.
“Ninataka kwenda kumshukuru Rais Kenyatta. Nina watoto wawili wa kike, ambao sasa wataweza kwenda shule na kusoma bure bwerere na hiyo ni kwa ukarimu wa chama cha Jubilee,” alisema Mutiria.
Mutiria pia aliongeza kuwa, atamshukuru kwa kitendo chake cha kuanza shughuli za ujenzi wa barabara za kuiunganisha Tharaka na maeneo mengineyo ya nchi.
“Kwa muda mrefu tulitengwa na tawala nyinginezo, lakini Serikali ya Uhuru imekuwa njema kwetu. Amekuja kututembelea kwa kutumia barabara zisizo na madaraja, na njia mbovu kabisa ambazo hazikuwahi kutumiwa na viongozi wengine,” alisema Mutiria.
Mkulima huyo alisema amefurahi zaidi, kwani watoto wake ambao wapo darasa la nane watanufaika na mpango wa elimu bure katika kupata elimu yao ya sekondari.
“Ndiyo maana nimepanga kumzawadia ng’ombe wangu wa pekee Rais Kenyatta,” alisema Mutiria ambaye amepanga kuianza safari yake Jumapili ya Agosti 20.
Katika safari hiyo ya aina yake, Mutiria ataambatana na wenzake wawili kwa ajili ya kumsaidia kubeba chakula cha ng’ombe huyo. Pia, aliongeza kuwa mtoto wake mmoja wa kike ataambatana naye kwa ajili ya kwenda Ikulu kumshukuru Rais Kenyatta.
“Ninawaomba viongozi wa Tharaka wanisaidie ili nionane na Rais Kenyatta, iwapo nitanyimwa kuonana naye” alisema Mutiria.
The Star.

No comments

Powered by Blogger.