Header Ads

Mugabe auza ng’ombe 600 kuisaidia AU



President Mugabe with the cheque
ADDIS ABABA- RAIS Robert Mugabe amebainisha kwamba, Zimbabwe imeuza ng'ombe 600 na kupata dola za Marekani milioni 1 (sh bilioni 2.2) kwenye mnada na kukabidhi fedha hizo kwa Wakfu wa Muungano wa Afrika kusaidia kumaliza utamaduni wa kutegemea fedha kutoka kwa wafadhili.

Rais Mugabe alisema kuwa, yeye binafsi alitoa ng'ombe 300 kutoka kwenye zizi lake, na raia wengine wa Zimbabwe wakaongeza ng'ombe wengine 300.
Akizungumza katika mkutano huo, Mugabe alisema mchango huo ni mdogo tu lakini ni ishara muhimu katika kujaribu kukomesha utegemezi wa Afrika kwa fedha za wafadhili.
“Kama Mwafrika na mkulima, kutoa ng'ombe ni jambo la kawaida kwangu, ikizingatiwa kwamba bara letu limebarikiwa na ng'ombe wengi na ng'ombe hutazamwa kama hazina ya utajiri,” alisema Mugabe.
Mugabe alikabidhi hundi hiyo ya dola milioni 1 kwa AU, wakati wa mkutano mkuu wa viongozi wa mataifa wanachama nchini Ethiopia. Mchango huo wa Zimbabwe, unakuja katika kipindi ambacho taifa hilo linakabiliwa na uhaba wa fedha na chakula.
Mwaka jana, watu zaidi ya milioni 4 nchini humo walihitaji chakula cha msaada baada ya mvua kutonyesha kwa kiwango stahiki. Hata hivyo, mwaka huu mavuno yamekuwa mengi na taifa hilo linatarajiwa kujitosheleza kwa chakula kwa mara ya kwanza katika miaka mingi.
Upinzani umelaumu Serikali kwa uhaba huo wa chakula, na kusema kwamba sera yake yenye utata ya kupokonya wazungu mashamba ilichangia kusambaratisha sekta ya kilimo.
Zimbabwe imelazimika pia kuanza kutumia hati za dhamana baada ya kuishiwa na dola za Marekani, fedha ambazo hutumiwa kwa biashara nchini humo. Kiwango cha juu cha mfumko wa bei kiliilazimu Zimbabwe kuacha kutumia dola yake mwaka 2009.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Zimbabwe, Simbarashe Mumbengegwi alisema ng'ombe hao walitolewa na watu waliofaidika kutokana na mageuzi katika sera ya mashamba nchini humo, kwa mujibu wa gazeti la Serikali la Herald.
Msaada huo ulikuwa ni ‘kuimarishwa’ kwa ahadi ya Mugabe ya mwaka 2015, kwamba angetoa ng'ombe 300.
Kwenye tovuti yake, Wakfu wa AU unasema huwa unaangazia mipango ya vijana na wanawake, na kuendeleza usawa wa jinsia.
Wakati wa kipindi chake kama mwenyekiti wa AU kati ya 2015 na 2016, Mugabe alitetea AU iwe ikifadhiliwa na Waafrika. Kwa sasa asilimia 60% ya bajeti ya umoja huo hutoka kwa wafadhili kutoka nje.

No comments

Powered by Blogger.