Header Ads

Ilani za uchaguzi zazua maneno Kenya



NAIROBI- MIJADALA mikali imezidi kupamba moto kwenye ulingo wa kisiasa nchini, baada ya Muungano wa Vyama vya Upinzani (NASA) pamoja na chama tawala, Jubilee, kushutumiana vikali kuhusiana na ilani.

NASA inayoongozwa na Raila Odinga, ndiyo ambao walioanzisha mashambulizi kwa Jubilee, baada ya kudai kuwa ilani ya Jubilee ina mapungufu mengi na isiyokuwa na maana yoyote kwa Wakenya.
Mara baada ya mashambulizi hayo, Jubilee wanaoongozwa na Rais Uhuru Kenyatta nao walijibu shutuma za wapinzani kwa kudai kwamba wamekuwa wakinadi malengo ambayo si ya kweli.
Awali, NASA walitoa taarifa iliyodai kwamba Jubilee wameshindwa kuwaeleza Wakenya kuhusu wao kushindw akutekeleza ahadi zao walizotoa kwenye ilani yao ya uchaguzi wa mwaka 2013, na kisha kudai kuwa ilani yao (Jubilee) iliyozinduliwa Jumatatu wiki hii inaakisi ahadi nyingi zilizofeli.
Seneta wa Kisumu, Anyang’ Nyong’o ambaye anaiwakilisha NASA, alisema kuwa Jubilee haipaswi kuaminika kuwa itaboresha uchumi wakati utawala wao ulishindwa kusimamia uchumi huo kwa miaka yote waliyokuwa madarakani.
“Kila sekta inapunguza wafanyakazi kuanzia kampuni za simu, benki hadi bima. Tazama bei ya unga, mfumuko wa uchumi ambao umesababisha mamilioni ya Wakenya kutomudu gharama za maisha,” alidai Nyong’o.
Lakini Jubilee kupitia kwa Katibu Mkuu wao, Raphael Tuju na Naibu Katibu Mkuu, David Murathe, walipuuza shutuma za NASA na badala yake waliwashutumu kwa kutoa ahadi zisizo za kweli kwa Wakenya kupitia ilani yao.
“Hivi ni kweli kwamba hatuna kitu tulichokifanya? Tumefanikiwa kutengeneza mradi mkubwa wa Standard Gauge ambao ni mkubwa kwa Afrika Mashariki na Kati katika kipindi cha miaka mitatu tu. Wao wamechagua kutoona hata yale ya kawaida,” alisema Tuju.











No comments

Powered by Blogger.