Header Ads

Daraja la Magara kuanza kujengwa Julai mwaka huu


Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Manyara, Mhandisi Bashiri Rwesingisa, akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani, wakati alipokuwa akikagua mahali ambapo litajengwa Daraja la Magara lenye urefu wa meta 84, wilayani Babati, mkoani Manyara, jana.



Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani, akitoa maelekezo kwa Mhandisi Christopher Saul (katikati), kutoka Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), mkoa wa Manyara wakati alipokuwa akikagua mahali ambapo litajengwa Daraja la Magara lenye urefu wa meta 84, Wilayani Babati, mkoani humo, jana.

Mwonekano wa sehemu ambapo Daraja la Magara lenye urefu wa meta 84 katika barabara ya Mbuyu wa Mjerumani-Mbulu yenye urefu wa kilomte 21 litakapojengwa. Mkataba wa ujenzi wake unatarajiwa kusainiwa mwezi Juni mwaka huu.



Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani, akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Mayoka kuhusu mkakati wa Serikali katika ujenzi wa Daraja la Magara wilayani Babati, mkoani Manyara, jana.

Serikali imesema ipo katika hatua za mwisho za kumpata mkandarasi atakayejenga Daraja la Magara lenye urefu wa meta 84 katika barabara ya Mbuyu wa Mjerumani-Mbulu yenye urefu wa kilometa 21 lililopo mkoani Manyara ambapo mkataba huo unatarajiwa kusainiwa Juni mwaka huu.
Akizungumza hayo jana kwa wananchi wa Kijiji cha Mayoka, wilaya ya Babati, mkoani humo, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani, aliwataka wananchi hao kutoa ushirikiano kwa mkandarasi atakayepatikana ili kurahisisha mradi huo kukamilika kwa wakati.
“Serikali inaendelea kukamilisha taratibu zake ili kumpata mkandarasi, sasa ombi langu kwenu ni kuhakikisha kuwa mnatoa ushirikiano kwa mkandarasi huyo pindi atakapofika eneo la kazi,” alisema Ngonyani.
Alibainisha kuwa Serikali imekuwa ikitenga fedha mwaka hadi mwaka, ili kuweza kukamilisha mradi huo ambapo kwa mwaka wa fedha 2017/18 zaidi ya Sh. bilioni 1 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa kilometa 1.2 za barabara sehemu ya mlima Magara ambayo itajengwa kwa kiwango cha zege.
Naye, Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Manyara, Mhandisi Bashiri Rwesingisa alimhakikishia Naibu Waziri huyo kumsimamia mkandarasi atakayepatikana katika ujenzi wa daraja hilo ili kuondoa kero na adha wanayopata wakazi wa Babati na maeneo jirani.
Aliongeza kuwa ujenzi wa daraja la Magara, pia utahusisha ujenzi wa barabara unganishi zenye urefu wa kilometa 2 kwa kiwango cha lami na kilometa 2 kwa kiwango cha Changarawe.
Daraja la Magara ni moja ya daraja litakaloleta chachu ya maendeleo kwa wakazi wa Arusha, Mbulu na Babati, kwani ujenzi wake utarahisisha huduma za usafirishaji na kukuza utalii kwa nchi kupitia Hifadhi ya Mbuga ya Manyara.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

 

No comments

Powered by Blogger.