Header Ads

Watano wafariki shambulio la kigaidi Westminister

Mshukiwa Westminster 

Polisi wakiwapatia huduma za kwanza majeruhi wa tukio la kigaidi lililotokea jana katika eneo la Bunge la Westminister.
 LONDON, Uingereza
WATU watano wamethibitishwa kufariki dunia na wengine zaidi ya 40 kujeruhiwa, baada ya mshambuliaji kuvurumisha gari na kuwagonga watu katika daraja la Westminister jijini hapa.

Mara baada ya kugonga kwa gari, shambuliaji huyo kisha alimdunga kisu ofisa wa polisi lakini akauawa kwa kupigwa risasi na polisi katika maeneo ya Bunge. Ofisa wa polisi aliyeuawa ametambuliwa kwa majina ya Keith Palmer, 48.
Waziri Mkuu, Theresa May amesema shambulio hilo lilikuwa ‘la ukosefu wa maadili’ na lilishambulia maadili makuu ya uhuru wa kufanya maamuzi, demokrasia na uhuru wa kujieleza. Polisi hawajafichua jina wala maelezo zaidi kumhusu mshambuliaji.
May alishutumu shambulio hilo na kusema juhudi kama hizo za kuvuruga maadili ya Uingereza hazitafanikiwa.
Aliwashukuru maafisa wa polisi waliofika eneo hilo baada ya tukio na kusema: "Sote tutasonga mbele pamoja, hatutayumbishwa na ugaidi na hatutakubali chuki na uovu kututenganishwa. Haikuwa ajali kwamba shambulio hili lilitekelezwa eneo hili.
Map
"Gaidi huyu aliamua kushambulia katikati mwa jiji kuu ambapo watu wa mataifa yote, dini zote na tamaduni zote hukusanyika kusherehekea maadili ya uhuru wa maamuzi, demokrasia na uhuru wa kujieleza."
May anatarajiwa kutoa hotuba baadaye leo katika Bunge la Commons.
Kaimu Naibu Kamishna wa Polisi ambaye anasimamia kitengo cha kukabiliana na ugaidi katika Polisi wa Jiji Kuu, Mark Rowley amesema anafikiria wanamfahamu mshambuliaji na kwamba huenda alihamasishwa na makundi ya kigaidi ya kimataifa yenye uhusiano na itikadi kali za Kiislamu.
Hata hivyo, hakutoa maelezo zaidi. Shambulio hilo lilitokea majira ya saa 14.40 (nane na dakika arobaini mchana kwa Uingereza) GMT jana, baada ya mshambuliaji mmoja aliyekuwa na gari la rangi ya kijivu aina ya Hyundai i40 alipolivurumisha gari hadi eneo la kutumiwa na wanaotembea kwa miguu kwenye Daraja la West Minister, karibu na Majengo ya Bunge.
Aliwaua watu wawili na kuwajeruhi wengine wengi. Baadaye aligongesha gari lake kwenye uzio nje ya Majengo ya Bunge. Baada ya matukio hayo, mshambuliaji huyo alikimbia, akiwa na kisu, hadi kwenye jengo la Bunge ambapo alikabiliwa na polisi.
Palmer ambaye hakuwa na silaha, alidungwa kisu na mshambuliaji huyo alifariki baadaye. Mshambuliaji huyo alipigwa risasi na kuuawa na polisi waliokuwa na silaha hapo karibu.
Rowley alitoa heshima zake kwa Palmer, na kusema: “Ni mtu aliyetoka kwake nyumbani leo kwenda kazini akitarajia kurejea nyumbani baada ya kumaliza zamu yake, na alikuwa na kila haki kutarajia kwamba hilo lingefanyika.”
Waziri wa Mambo ya Nje, Tobias Ellwood, mwanajeshi wa zamani ambaye kaka yake aliuawa katika shambulio la kigaidi la Bali mwaka 2002, alijaribu kumpa Palmer huduma ya kwanza.
Mwanamke mmoja alifariki baada ya kugongwa na gari la mshambuliaji huyo kabla ya gari hilo kufika eneo la majengo ya Bunge. Alithibitishwa kufariki na daktari katika hospitali ya St Thomas'.
Watu wakiwa karibu na gari lililogongeshwa kwenye ua
BBC




No comments

Powered by Blogger.