Header Ads

Zuma adaiwa kuwa na mpango wa kuhamia Dubai



Je, Rais Zuma ana mipango ya kuhamia Dubai?
Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma
JOHANNESBURG, Afrika Kusini
HALI imezidi kuwa tete kwa Rais Jacob Zuma, baada ya kuibuka kwa kashfa mpya ambapo wakosoaji wake wameeleza kwamba ana mpango wa kuhamia Dubai kwa ajili ya kuishi huko hivi karibuni.

Hayo yanajiri, baada ya kubainika kwa mawasiliano kupitia barua pepe ambazo zimechapishwa na gazeti moja nchini, zinazoonesha uhusiano mkubwa kati ya Rais Zuma na familia yenye utata ya Gupta, kuhusu madai hayo ya kuhamia Dubai.
Wakati chama tawala nchini cha ANC kikikumbwa na vita vya ndani kwa ndani, barua pepe hizo zinatarajiwa kuibua mjadala mkali kwani zinafichua mipango ya Rais Zuma wa kuhamia Dubai.
Barua pepe hizo baina ya mwanawe wa kiume, Duduzane, na vigogo wa kampuni inayomilikiwa na familia ya Gupta, zinashirikisha barua moja iliyotumwa kwa familia ya kifalme mjini Dubai, ambapo Zuma anasema angetaka kuwa na makao ya pili huko Dubai.
Madai hayo yanaibua mjadala wa iwapo Rais Zuma anajiandaa kubwaga manyanga, kwani chama chake nacho kinaonekana kumgeuka.
Hata hivyo, madai hayo yamekanushwa vikali na Msemaji wa Rais Zuma, ambaye amepuuza barua pepe hizo na kudai kuwa ni uvumi na uchokozi kwa kiongozi huyo.
Hayo yakiarifiwa, ombi la kutokuwa na imani na Rais Zuma limewasilishwa kwa Kamati Kuu ya chama cha ANC inayokutana mjini Pretoria ikiwa ni mara ya pili kwa ombi hilo kuwasilishwa.
Wanachama wa ANC ambao wanampinga Rais Zuma, kwa mara nyingine tena wanajaribu turufu yao, lakini huenda wanchama wa kamati hiyo watiifu kwa Zuma wakaangusha muswada huo.
Mbali na kuwasilishwa kwa maombi hayo kwa kamati kuu, bado kuna kesi inayoendelea katika Mahakama ya Katiba iwapo wabunge wataruhusiwa  kura ya siri ya kwa muswada wa kutokuwa na imani na Zuma. Kamati hiyo inatarajiwa kuamua atakayemridhi Zuma ifikapo Desemba mwaka huu.


No comments

Powered by Blogger.